Tovuti za Tanzania
 

Uzinduzi wa albam ya Safari 2005 Diamond Jubilee

Tarehe 26 mwezi wa nane mwaka 2005 siku ya Ijumaa ilikuwa siku kubwa sana kwa wanatwanga na kupepeta pale walipozindua albam yao ya saba katika muziki wa dansi. Siku yenyewe ilikuwa tulivu sana kutwa nzima na jioni ilipowadia watu walikuwa katika pilika pilika za kujiupara tayari kwenda kushuhudia kile ambacho kwa takribani mwezi mzima kilikuwa kinatangazwa kwenye vyombo vya habari

Nilipata nafasi ya kwenda kushuhudia uzinduzi huo na nilifika mitaa ya Diamond Jubilee kama kwenye saa mbili na nusu au tatu kasorobo hivi. Nikajongea kwenye tiketi na kupata tiketi yangu na mamsapu wangu maana siku hiyo alinipana ile mbaya niende naye kwani siku zote nilikuwa namkacha safari hii hakukubali. Basi tukaingia ndani baada ya kuonyesha tiketi zetu mlangoni Muda huo ukumbi ulishaanza kujaa watu tukaenda mbele kidogo kwa bahati nzuri tukafanikiwa kupata viti karibu na ukuta ambao unatenganisha kati ya waliotoa kiingilio cha pili na cha kwanza, cha kwanza kikiwa ni VIP na cha pili ni kile cha akina sisi.


Kwa kweli kwa wakati huo kulikuwa hakuna bendi yoyote inayoburudisha ila niliweza kuwaona vijana wa benchmark wakiwa na video kamera zao huku pembeni mwa kuta za Diamond kukiwa na screen kubwa mbili ambazo zilikuwa zinaonyesha LIVE nini kinachoendelea pale ukumbini.

Kwa kuwa Onyesho lilikuwa alijaanza basi nikaenda kutafuta cha kulumangia. Nilirudi kwenye siti yangu tayri kuangalia nini kinachoendelea na kweli mra akaja MC Maumatha na kuwakaribisha watu wote pale na kutoa ratiba ya burudani kwa siku hiyo. MC aliwakiribisha wana African Revolution band wana Diko Diko kuanza kutumbuiza. wana Diko bila kupoteza muda waliingia na kuanza kuwasha moto. kwa kweli watu waliwashangilia sana hasa kwa shoo zao ambazo zilikuwa zimetulia ile mbaya.

Kwa kweli wacheza shoo wa Diko sio mchezo hasa kina Rukia Bruno na Asha huku Grace na Aliyah nao wakijipinda kama nyoka aina ya Anaconda. Albam ya hawa African revolution ni hatari yaani kama haujaipata tafari nenda sasa dukani kabla haijaisha maana unakosa uhondo. Diko diko waliendelea kwa muda na ilipotimu saa tano kasorobo hivi mambo yakaanza Mc aliishika kipaza sauti na kumkaribisha Mkurugenzi wa ASET Asha Baraka ili naye aseme machache na wakati huo huo kukaribisha mgeni rasmi ambaye alikuwa mmoja wa wagombea ubunge katika uchaguzi unaokuja baada ya kukaribishwa naye aliongea machache na kuizindua albam kwa kuonyesha mfano wa CD ambayo itakuwa na jina la safari 2005

Wapenzi wa twanga walimshangilia mgeni rasmi na yeye hakutaka makuu aliomba wana twanga waingie stegini na kuanza kutumbuiza. Basi kila mtu hakujua nini kinatokea mara tukasikia tututututuutu tututuuutuuu eh! kila mtu akawa anaangalia huku na huku eh nini tena hicho mara kwa upande wa kushoto eh skuta pikipiki duh wapigaji wa twanga wanaingia na Bajaj duh wanaingia wawili wawili, wakiongozwa na Baba Diana Abuu Semuando huyo kasimama kwenye bajaj kuangalia vizuri tunamuona MCD naye huyo yupo na mzee wa Bass gitaa Jojoo jumanne Victor mkambi huyo naye anakuja na bajaj nyingine kwa kweli pale mbele ya jukwaa ni fujo tupu bajaj zinapiga misele ndani ya ukumbi mabaunsa wanazunguka huku na huku kuweka ulinzi mkali duh hawa madereva wa Bajaj ni mafundi sana maana wanapiga no linda humu humu ndani ya ukumbi kwa kweli ni ajabu sana

Wapigaji wa twanga wanatelemka kwenye hizo Bajaj na kuelekea kwenye jukwaa tayari kutuletea burudani. watu wanabaki wanashangaa na kusema ama kweli twanga safari hii wameamua sio mchezo. Linapigwa sebene pale watu wanatupa macho huku na huku kuangalia nani wanakuja safari hii, mara kwa upande ule ule wa kushoto wanaingia waimbaji wa twanga wakiongozwa na akina Chokoraa, Charles Baba, Diouf, Amigoras, Lwiza Mbutu, Salehe kupaza na Banza Stone ambao wanakuja kwa staili ambayo hatujawahi kuiona katika maonyesho yao, alafu kilichopendezesha sasa walikuwa wametilia mavazi meupe yaani suruali nyeupe na mashati meupe huku wakiwa wameuramba mkanda mweusi ee bwana ee walitoka bomba ile mbaya na chini wamekula kiatu cheusi kilichong'arishwa vizuri sana. huku wakiendelea kulisakata sebene lile watu waliwashangilia sana hasa Banza Stone ambaye alikuwa anajituma ile mbaya huku Diouf naye akilisakata hilo sebene kwa makini sana.

Sasa ikaingia zamu ya wacheza show ee bwana ee! kweli hii safari maana wacheza shoo waliingia na staili ya traffic kwa kweli walipendeza sana hasa kofia zao na kina dada zile mini sketi zao huku wavulana wakiwa na nguo nyeupe tupu pamoja na kofia nyeupe, kwa kweli tuliopata nafasi ya kuona uzinduzi huu tulipata burudani ya kukata na shoka. Baada ya show hiyo ya traffic twanga walianza na wimbo mpya unaoitwa Safari ambao umebeba Albam yenyewe ama kweli Twanga ni kisima cha burudani maana kwa ujumla wanamuzi wote walijituma sana kuonyesha uwezo wao na kweli tulipata burudani safi sana siku hiyo.

Twanga walipiga nyimbo nyingine tano na watu waliwashangilia sana. Baada ya nyimbo hizo Twanga walienda kwenye mapumziko kidogo hiyo ilikuwa kama kwenye saa saba na nusu usiku hivi hapo sasa MC akatangaza kuwa ni zamu ya baba ya muziki msondo Ngoma kutumbuiza watu walifikiri utani mara tukawaona hao msondo ngoma wakiingia kwenye stage na uniform zao bomba nikamuona Mabele akishikilia gitaa la solo na Ngurumo naye huyo mambo yakaanza wimbo wa talaka yangu utatoa ndiyo ulikuwa wa kwanza watu walishindwa kujizuia wakavamia kwenye dancing floor na kuanza kusakata msondo ngoma.

Kweli hawa jamaa wa msondo ni baba wa muziki hapa Tanzania maana jinsi walivyokuwa wanapiga we acha tu. Msondo walipiga nyimbo kama tatu hivi na baada ya hapo wana wa kutwanga na kupepeta waliingia tena jukwaani safari hii walipiga zile nyimbo za albam zilizopita, walianza na wimbo wa Mtu pesa wapenzi waliivamia dancing floor na kuanza kutwanga na kupepeta kwa nguvu zote.

Twanga waliendelea kuwapa burudani wapenzi waliofika kwenye uzinduzi huo mpaka kwenye muda wa sa tisa na nusu hivi ndiyo ikawa mwisho wa onyesho hilo. Baada ya Twanga kumaliza taratibu nilimvuta mwenzi wangu tukatoka nje na kwa bahati mabasi yalikuwepo usiku huo tukapanda basi yaani daladala mpaka mahome UZINDUZI ULIFANA SANA MTU KIBAO. Picha za uzinduzi huo zinapatikana hapa

 
   
     
Matangazo
   
     
All rights reserved by ASET
Powered by Benton MEDIA